kabesejr blog

kabesejr

albino

Thursday, September 13

AZAM WANAIONJA KAITABA MBOVU LEO


Kikosi cha Azam


AZAM leo itafanya mazoezi kwenye Uwanja wa Kaitaba, Bukoba ili kuuzoea kabla ya kushuka dimbani kesho kumenyana na wenyeji, Kagera Sugar kwenye Uwanja huo huo ‘mbovu ile mbaya’ katika mchezo wa awali wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara.
Azam jana ilifanya mazoezi kwenye Uwanja wa seminari ya Mtungamo na zaidi wachezaji walikuwa wanalalamikia baridi kali, tofauti na hali ya joto waliyoizoea Dar es Salaam.
Mshambuliaji wa zamani wa Kagera Sugar, Philipo Alando, ambaye kwa sasa ni mmoja wa viongozi wa klabu hiyo ya Chamazi, ndiye ameongoza msafara wa timu Bukoba, kwa yeye ni mwenyeji huko, lakini pia John Bocco, Luckson Kakolaki na Gaudence Mwaikimba si wageni huko.
Alando ambaye alistaafu soka akiwa na jezi ya Azam miaka miwili iliyopita, amepewa jukumu la kuhakikisha anaiongoza Azam kubeba pointi sita za mwanzoni za Ligi Kuu katika mechi mbili za Kanda ya Ziwa, baada ya mechi ya keshokutwa watakwenda Mwanza, kuivaa Toto African.
Kocha Mkuu wa Azam FC, Mserbia Boris Bunjak amesema timu yake ipo tayari kwa Ligi Kuu, lakini tu amehadharisha marefa wachezeshe kwa haki.
Bunjak alikerwa mno na marefa waliochezesha mechi ya Ngao ya Jamii Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam juzi kwamba waliwabeba wapinzani wao Simba SC.
Mechi hiyo ilichezeshwa na Martin Sanya, aliyeisaidiwa na Omar Kambangwa na Ephron Ndissa, wakati refa wa akiba alikuwa Oden Mbaga na Kamisaa Omary Kasinde.
Akizungumza na BIN ZUBEIRY baada ya mechi hiyo, Bunjak alisema kwamba marefa hao walionyesha mapungufu makubwa kwa kuwapendelea wazi wazi Simba na hata wakafanikiwa kutoka nyuma kwa mabao 2-0 na kushinda 3-2.
“Nafikiri tulicheza mechi nzuri, tukaongoza 2-0, baada ya hapo tukapoteza nafasi nzuri za kufunga, lakini siamini kwa nini refa alitoa penalti dakika ya mwisho(kipindi cha kwanza), kwa sababu ule mpira ulikuwa kwenye himaya ya wachezaji watatu kutoka nyuma, unaweza kuonaje nani aliucheza kwa mkono.
Bao la pili pia, pia ulikuwa msaada mkubwa, niliandaa timu yangu kucheza dhidi ya wachezaji 10, siyo wachezaji zaidi, mimi si kocha nayeandaa timu kucheza dhidi ya wachezaji wengi, naweza kufanya nini, tulicheza vizuri, tulipoteza nafasi, refa alitunyima penalti mbili, asilimia 100, naweza kufanya nini, labda hii ni soka ya Tanzania tu.
Nitafanya nini, huu ni uzoefu wangu wa kwanza ofisini tena, lakini nimeshashangazwa sana, Simba ni timu kubwa, Simba ni timu nzuri, lakini leo Azam imecheza vizuri, Azam ilistahili kushinda taji,”alisema.
Kocha huyo alionyeshwa kuridhishwa na bao moja moja tu la Simba, la tatu ambalo alisita kulizungumzia kabisa katika malalamiko yake.
Azam juzi iliiruhusu Simba SC kutoka nyuma kwa mabao 2-0 na kushinda 3-2, hivyo kutwaa Ngao ya Jamii, kwa mara ya pili mfululizo Uwanja wa Taifa, Dar e s Salaam.
Shujaa wa Simba jana alikuwa ni kiungo Mwinyi Kazimoto aliyefunga bao la ushindi dakika ya 78 kwa shuti kali la mbali baada ya kumchungulia kipa wa Azam, Deo Munishi ‘Dida’ amekaaje.
Hadi mapumziko, Azam walikuwa mbele kwa mabao 2-1, yaliyotiwa kimiani na John Raphael Bocco ‘Adebayor’ na kipre Herman Tchetche, wakimtungua kipa namba moja Tanzania, Juma Kaseja.
Bocco alitangulia kufunga dakika ya tano ya mchezo huo, baada ya kupigiwa kona fupi na Abdi Kassim ‘Babbi’, akatoa pasi kwa Abdulhalim Humud ambaye alimrudishia mfungaji huyo akafumua shuti kali la chini likajaa nyavuni pembezoni mwa lango kulia.
Bocco ambaye alikuwa mwiba mchungu kwa safu ya ulinzi ya Simba SC leo, alimtoka Amir Maftah upande wa kulia wa Uwanja na kuingia ndani kabla ya kutoa krosi fupi kwa Kipre aliyemtungua Kaseja na kuipatia Azam bao la pili dakika ya 35.
Simba ilipata bao lake la kwanza dakika ya kwanza ya muda wa nyongeza, baada ya kutimu kwa dakika 45 za kipindi cha kwanza, mfungaji Daniel Akuffo kwa penalti, baada ya Said Mourad kuunawa mpira kwenye eneo la hatari.
Kipindi cha pili Simba walirudi na nguvu zaidi na kuamua kushambulia kwa mipira ya pembeni, ikiwatumia Mrisho Ngassa na Emanuel Okwi ambao walikuwa wakibadilishana reli. 
Kwa staili hiyo, haikushangaza Simba ilipotumia dakika 45 za mwisho kwa kufunga mabao mawili yaliyowatoa nyuma kwa 2-1 na kuibuka kidedea kwa ushindi wa 3-2.
Emanuel Okwi alimchambua kama karanga Erasto Nyoni na kuingia ndani kabisa akiwatoka mabeki wengine wa Azam, kabla ya kuujaza mpira nyavuni kwa shuti kali na Kazimoto akamaliza kazi dakika ya 78.
Kwa ujumla katika mchezo huo, Azam ilitawala kipindi cha kwanza na ilikosa mabao mawili zaidi ya wazi kupitia kwa Himid Mao na Kipre, lakini kipindi cha pili Simba walitawala mchezo na kama wangekuwa makini, nao wangeweza kuvuna mabao zaidi. 
Naibu Waziri wa Kazi, Makongoro Mahanga alimkabidhi ngao Nahodha wa Simba, Juma Kaseja baada ya mechi hiyo, ambaye alikwenda kushangilia na wachezaji wenzake na mashabiki wa timu hiyo.

No comments:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...